Home KITAIFA RAIS DK.SAMIA : SERIKALI ITAENDELEA KUSHUGHULIKIA CHANGAMOTO ZA WAKULIMA.

RAIS DK.SAMIA : SERIKALI ITAENDELEA KUSHUGHULIKIA CHANGAMOTO ZA WAKULIMA.

Ruvuma

 RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan amesema serikali itaendelea kushughulikia changamoto za wakulima na kumuagiza Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe kufanya  uchunguzi wa  madai ya wakulima  wa kahawa  kukatwa fedha kinyemela  na vyama vya vikuu vya ushirika.

Pia imemuahizi kuhakikisha anakuja na mfumo wa wazi utakao wanufaisha wakulima hao, kuondoa ujanja unaofanyika sasa.

Kauli hiyo ameitoa leo Septemba, 24 2024 alipotembelea shamba la uzalishaji wa Kahawa la AVIV mara baada ya uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi  wa maghala  28 ya kuhifadhi mazao ya nafaka yaliyo chini ya Wakala wa hifadhi ya Chakula (NFRA) Wilayani Songea Mkoani Ruvuma katika muendelezo wa ziara yake ya siku sita mkoani huko.

Amesema mafanikio yaliyopo  katika sekta ya kilimo hayatokei kwa bahati mbaya bali ni kutokana na juhudi zilizofanywa na serikali.

Serikali imefanya maboresho kwa wakulima kwa kupunguza makato na tozo ili mkulima anufaike na jasho lake, kuanzisha mnada wa kahawa kwa njia ya mtandao mkulima kunufaika kwa bei ya bei, kuongeza ufanisi katika malipo ya wakulima.

“Kule nyuma mkulima alikuwa akipeleka kahawa yake katika chama kikuu cha ushirika mpaka iuzwe apate mapato yake sio chini ya miezi miwili, lakini leo mkulima analipwa sio chini ya siku mbili au tatu, anapeleka mazao yake na kulipwa pesa yake.

“Kila penye mafanikio hapakosi changamoto, natambua eneo hilo la Vyama Vya ushirika  Waziri ni malalamiko ya wananchi  kwa sasa, kwa kuwa kahawa imepanda bei na wanauza kwa bei nzuri, wameanza kuwakata makato kinyemela,” amesema.

 Alimuagiza Bashe alifuatilie hilo, kuwepo na mfumo ambao  mkulima akiuza  unaonesha kila kitu  kilichouzwa na kilichobaki.

“Waziri mfumo  uoneshe  mkulima akiuza hapa, makato ni  haya na kinachobaki ni cha kwangu kuwe na mfumo wa wazi ili wakulima wanufaike na  mazao yao hivyo ujanja ujanja wa leo kukata hiki kesho kile hahaaaaa..  haufai, kuwe na mfumo unaoeleweka,” amesema

Amesema zao la kahawa pekee limeongezeka katika uzalishaji kutoka tani 65,000 hadi kufikia tani 85,000 hivyo kuingiza nchini  dola za kimarekani milioni 250.

Ameitaka Wizara ya Kilimo kuhakikisha wawekezaji waliopo mbali wanayoyafanya katika kurudisha kwa jamii za wanahusisha kurithisha  ujuzi na teknolojia hususami za umwagiliaji zinazo tumika katika sekta hiyo ili kuwezesha wananchi kuwa na kilimo chenye tija kwa maslahi ya vizazi vijavyo.

Rais Dk. Samia amewataka  wakulima kutumia fursa ya kupanda kwa bei ya kahawa, kuhifadhi fedha ili wasitaabike kipindi bei itakapo shuka.

“Misimu ikiwa mizuri na bei ikiwa nzuri tuwe na mifumo ya kujiwekea akiba ili mabadiliko ya tabianchi yanapotokea tuwe na Akiba,” amesema.

Pia ameitaka Wizara ya Kilimo kujipanga vyema na masharti yanayotolewa na masoko ya kimataifa ya kahawa hasa lile la uzalishaji bila kukata misitu.

“Bodi ya kahawa kujipanga vizuri na masharti yanayotolewa na soko la Ulaya kutambulika kwani mkikata misitu na kupanda  kahawa hawatainunua kwa sababu ya kuharibu mazingira, pia hakikisheni mashamba hayo yanatambulika na ukubwa wake na kwenda kuyasajili ili wajuie kahawa wanayonunua inatokana na mashamba ya Tanzania,” amesema.

 Agizo hilo lizingatiwe ili serikali isije ikakosa  soko zuri la Kahawa Ulaya.

Amesema Serikali imeongeza uwekezaji kwa zao la kahawa  kwani imekuwa ikitoa kipaumbele kwenye kilimo na imekuwa ikifanya kwa vitendo ikiwemo kuongeza bajeti ya wizara kwani mwaka wa fedha 2020/2021 ilikuwa sh. Bilioni 460 na sasa 2024/205 ni sh. Bilioni trioni 1.2 kwa sekta ya kilimo pekee.

Amesema lengo ni kukuza mazao ya kilimo  kuweza kuuza nje na kupata fedha ya kigeni. Ongezeko la bajeti limeiwezesha serikali kuongeza idadi ya maofisa ugani, uzalishaji wa mbegu bora za kahawa ambapo kwa mwaka wanazalisha miche  takribani milioni 20 na kuigawa  bure kwa wakulima kuongeza uzalishaji wa zao hilo.

 Ameitaka wizara ya kilimo kusimamia hilo kwani wanaposema wakulima wawekewe skimu ya umwagiliaji ili wazalishe  kahawa  maeneo hayo ni ya kuyaangalia ili mbegu zinazokwenda kwa wakulima ziwe zinakubalika.

ULIPAJI FIDIA

Rais Dk. Samia  amesema hakuna mwananchi aliyeguswa na mradi unaotekelezwa na serikali  asilipwe fidia.

 Amesema ingawa inaweza kuchelewa  lakini serikali  itahakikisha inamlipa kila mwananchi  haki yake anayostahili.

“Ninawashukuru wananchi kwa kupisha miradi iendelee  mkisubiri fidia zenu hivyo kila anayepaswa kulipwa atapata fidia, hakuna mradi utakaopita serikali ikachukua ardhi bila kulipa fidia ya mtu tunaweza kuchelewa kulipa lakini tutalipa zote,” amesema.

 Amewataka wananchi hao kufanya kazi kwa kulima mazao mengi, kuongeza uzalisha na kuuza nje kwa wingi kupata fedha nyingi kufanya mambo yao ya ndani.

Amesema miradi mingi inayotekelezwa ni fedha za kukopa nje hivyo wanashindwa na mapato ya ndani kulipa kwa haraka fidia lakini kadri wanavyokusanya ndivyo wanavyolipa.

MRADI WA MAJI MTYANGIMBOLE

Akiweka jiwe la msingi katika mradi wa maji Mtyangimbole Songea mkoani Ruvuma alisema  ziara yake imedhamiria kuweka jiwe  la msingi kwa miradi 30 inayoendelea  mkoani humo hivyo mradi huo unakwenda kuhudumia vijiji vitatu hivyo anaamini maji yatabaki na kwenda katika vijiji vingine.

Amesema anaamini baadhi ya miji watakuwa wanapata maji kwa ukamilifu  ukiwemo mji wa Songea ambao utapata kwa asilimia 100 hivyo anatarajia kipimo cha Ilani ya Uchaguzi watakuwa wamevuka.

Amesema ikifika mwakani lengo la CCM kuwa vijiji vyote nchini vipate maji kwa asilimia 85 litakuwa limetimia au kuzidi huku mjini kwa asilimia 95.

“Nilikuwa naangalia mfumo wa mradi huu ambao chanzo chake kikubwa ni mto Kibondo, chanzo kile kinatoa maji mengi nikasema  yatabaki na vijiji vingine watapata, ombi langu kwenu ni kutoharibu kile chanzo cha maji, ule ndio uhai wenu, maji haya yatatumika kwa matumizi ya binadamu wanyama na kilimo kwa baadhi ya maeneo.

“Niwaombe tusiharibu chanzo kinachotupa uhai huu, kule mtoni twende tukatumie lakini kuwe na ulinzi wa kutosha, walinzi wa kwanza muwe wananchi na sio watu wa maji, watu wa maji kazi yao kuangalia maji yakowapi watafasnya nini yaweafikie wananchi,” amesema.

Ametoa miezi mitatu kwa Waziri  wa Maji, Jumaa Aweso na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, kuhakikisha maji yanafika kwa wananchi.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here