Home KITAIFA WANANCHI WAJIOKEZA KWA WINGI KWENYE BANDA LA TPDC 77

WANANCHI WAJIOKEZA KWA WINGI KWENYE BANDA LA TPDC 77

Dar es Salaam

KATIKA Maonyesho ya 48 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba), wananchi wamejitokeza kwa wingi katika banda la Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) wakitaka kujua zaidi kuhusu matumizi ya gesi asilia.

Afisa Uhusiano wa TPDC, Francis Lupokela, akizungumza na kwenye maonyesho hayo amesema kuwa wananchi wengi wameonesha nia kubwa ya kujua jinsi gesi asilia inavyoweza kutumika katika maisha yao ya kila siku ikiwamo na viwanda.

“Katika maonyesho haya, tumeona mwitikio mkubwa kutoka kwa wananchi wanaotaka kufahamu zaidi kuhusu matumizi ya gesi asilia. Wananchi wanataka kujua jinsi ya kutumia gesi asilia majumbani mwao na pia katika shughuli za kibiashara.

“Wengi wao wanatamani kuona upatikanaji wa gesi asilia ukiongezeka katika sehemu mbalimbali hatua mbayo wanaamini kuwa itaweza kuwaokolea gharama na kutunza mazingira jambo ambalo sisi TPDC tumelipokea,” amesema Lupokela.

Lupokela ameeleza kuwa matumizi ya gesi asilia yana faida nyingi ikiwemo kupunguza gharama za nishati na kusaidia kuhifadhi mazingira. Alibainisha kuwa TPDC imejipanga kuhakikisha gesi asilia inafikishwa kwa wananchi wengi zaidi kwa gharama nafuu.

“TPDC imejipanga kuhakikisha tunafikisha gesi asilia kwa wananchi kwa gharama nafuu na kwa usalama. Tunaendelea na jitihada za kuongeza miundombinu ya kusambaza gesi ili iweze kuwafikia wananchi wengi zaidi,” aliongeza Lupokela.

Katika banda hilo, wananchi mbalimbambali walipata fursa ya kuona mifano ya matumizi ya gesi asilia katika kupikia, kuendesha magari, na kuendesha mitambo mbalimbali ya viwandani. Pia walipata elimu kuhusu usalama wa matumizi ya gesi asilia na jinsi inavyoweza kuboresha maisha yao ya kila siku.

“Haya maonyesho ni fursa muhimu kwa wananchi kupata elimu na kujua zaidi kuhusu gesi asilia. Tunawahimiza watembee katika banda letu ili wapate taarifa sahihi na kujionea wenyewe manufaa ya gesi asilia,” amrsema Lupokela.

“Elimu niliyoipata hapa imenisaidia kuelewa jinsi gesi asilia inavyoweza kupunguza gharama za nishati na kuchangia katika kuhifadhi mazingira, hivyo elimu hii ni muhimu iwapo itawafikia watu wengi zaidi ili kuchochea utunzaji wa mazingira,” amesema mmoja wa wakazi hao.

Maonyesho ya Sabasaba yanayoendelea yamekuwa ni jukwaa muhimu kwa TPDC kuwasilisha huduma na bidhaa zake kwa wananchi, huku ikiendelea na jitihada za kuongeza ufahamu na matumizi ya gesi asilia nchini.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here