Home KITAIFA SERIKALI KUTATUA CHANGAMOTO ZA WAZABUNI NA WAKANDARASI

SERIKALI KUTATUA CHANGAMOTO ZA WAZABUNI NA WAKANDARASI

Na Chedaiwe Msuya, Dodoma

SERIKALI imeeleza  kuwa katika bajeti ya mwaka 2023/24, ilitenga jumla ya shilingi bilioni 600 kwa ajili ya kulipa madeni ya wazabuni, wakandarasi, watumishi na watoa huduma mbalimbali ili kupunguza mzigo wa madeni na kuimarisha utendaji wa miradi ya Serikali.

Hayo yameelezwa Agosti 29, 2024 bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Hamad Hassan Chande , alipokuwa akijibu swali la Bupe Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum, aliyetaka kujua ni lini Serikali itawalipa wazabuni na wakandarasi waliotoa huduma mbalimbali katika Mkoa wa Rukwa, ambao hawajalipwa kwa kipindi cha miaka mitano.

Chande amesema kuwa Serikali itawalipa wazabuni na wakandarasi waliotoa huduma mbalimbali na kueleza kuwa hadi kufikia Juni 2024, jumla ya shilingi 491,254,100,645.65 zimetolewa kwa ajili ya kulipa madeni ya wazabuni na wakandarasi nchini kote. 


“Kati ya kiasi cha shilingi 88,629,271.20 zilitolewa kulipa wazabuni na wakandarasi wa Mkoa wa Rukwa. Hata hivyo, kiwango hiki bado kimeonekana kuwa kidogo ukilinganisha na mahitaji ya malipo katika mkoa huo, jambo ambalo katika mwendelezo wa utekelezaji wa miradi muhimu ya maendeleo,” amefafanua MChande.


Vile vile, Chande amejibu swali la Constantine John Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini, aliyetaka kujua kuhusu malipo ya posho za nyumba na majukumu kwa watumishi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (CKHT) ni lini serikali itawalipa watumishi hao ambao hawajalipwa tangu mwaka 2020.


Chande amesema  kuwa Wizara ya Fedha imepokea na kuhakiki madeni ya watumishi wa CKHT yenye thamani ya shilingi 5,430,613,831 na kuwa taratibu za kushughulikia malipo ya madeni hayo zinaendelea, na ahadi ilitolewa kuwa malipo yatatekelezwa katika mpango wa bajeti wa mwaka 2024/25.


“Serikali imejipanga kikamilifu kushughulikia suala hilo na kwamba malipo hayo yatatekelezwa ndani ya muda uliopangwa na kutambua umuhimu wa motisha kwa watumishi na itaendelea kuhakikisha kuwa haki zao zinaheshimiwa na kulindwa, na kwamba ucheleweshaji wa malipo hautajirudia tena katika siku zijazo,”amesema Chande

Ameongeza kuwa serikali imeweka mipango madhubuti ya usimamizi wa fedha, kuhakikisha uwazi katika usimamizi wa posho na madeni, na kuongeza ufuatiliaji wa karibu kuhusu utekelezaji wa bajeti ili kuepusha ucheleweshaji wa malipo.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here