Home KITAIFA SERIKALI ITAENDELEA KUTUMIA TEHAMA KUKUZA MAENDELEO – DK. BITEKO

SERIKALI ITAENDELEA KUTUMIA TEHAMA KUKUZA MAENDELEO – DK. BITEKO

📌 Lengo ni kuimarisha uchumi wa kidijitali

📌 Sekta binafsi yatakiwa kuchangamkia fursa

📌 Azindua Mpango wa Ujuzi wa Kidigitali kwa Wote – Digi Truck

Dar es Salaam

SERIKALI itaendelea kutoa kipaumbele katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano ili iweze kuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya kiuchumi kama inavyoelekezwa katika Dira ya Taifa ya 2025, Sera ya Maendeleo ya TEHAMA ya mwaka 2016 na Ilani ya CCM 2020-2025.

Hayo yamebainishwa leo Agosti 24, 2024 jijini Dar es Salaam na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto Biteko wakati akimwakilisha Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwenye uzinduzi wa mpango wa Ujuzi wa Kidigitali kwa wote (DigiTrack) uliowezeshwa na Huawei na Vodacom Foundation.

Amesema kuwa, Serikali inahamasisha matumizi ya TEHAMA ili kuwezesha wananchi hususani vijana na kizazi kijacho kushindana katika uchumi wa dunia.

“Kwa kuimarisha elimu ya TEHAMA, tunajenga jamii yenye ujuzi wa kutumia teknolojia kwa ufanisi, kubuni suluhisho za ubunifu, na kuchangia katika uchumi wa kidijitali. Hii itasaidia katika kuhakikisha kwamba maendeleo ya kidijitali yanakutanisha kila mmoja, bila kujali hali ya kiuchumi,” amesema Dk. Biteko.

Ameongeza kuwa, Serikali inayoongozwa na Rais Samia itafanya kila linalowezekana kuhakikisha kwamba wawekezaji wanakuwa msaada katika kubadilisha hali maisha ya watu kupitia nyanja mbalimbali ikiwemo TEHAMA huku pia wawekezaji hao wakinufaika na uwekezaji wao.

Dk. Biteko amesema uchumi wa kidijitali ni muhimu katika kuleta maendeleo kwa kuongeza ufanisi katika uzalishaji na na kuleta fursa na mapato ya ziada kwa wananchi.

Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Jerry Silaa amewapongeza Huawei na Vodacom kwa kuja na teknolojia ya Digi Truck ambayo inakwenda kuwa msaada kwa vijana wengi nchini ambayo itafika kila sehemu ili vijana wengi wajifunze.

Akizungumza katika hafla hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Philip Besiimire amesema kwa kushirikiana na Huawei watapeleka huduma hiyo ya kidijitali katika kila pembe kwa watanzania kutoa elimu hiyo hususani kwa vijana ili kuwezesha kizazi cha kisses kinachoendana na mabadiliko ya kisayansi na kibunifu.

Teknolojia hiyo iliyozinduliwa leo kutoka kampuni ya Vodacom Tanzania na Huawei itawezesha wananchi kupata elimu na ujuzi wa TEHAMA.

Hafla hiyo imehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali na wadau wa TEHAMA kutoka ndani na nje ya nchi ili kujionea uzinduzi huo muhimu.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here