Home AFYA WATOA ELIMU YA AFYA KWA NGAZI YA JAMII KUHUSU UGONJWA MPYA WA...

WATOA ELIMU YA AFYA KWA NGAZI YA JAMII KUHUSU UGONJWA MPYA WA MPOX

Mwanza

WAHUDUMU wa Afya ngazi ya jamii wameaswa kutoa elimu kwa umma kufahamu namna ya kujikinga dhidi ya ugonjwa wa Mpox uliotangazwa hivi karibuni na Shirika la Afya Duniani kuwa janga la kimataifa.

Wito huo umetolewa leo Agosti 21, 2024 kwa wahudumu wa Afya ngazi ya jamii katika wilaya ya Nyamagana Jijini Mwanza na Mratibu wa oparesheni za dharura kwa Afya mkoani Mwanza, Sia Urassa akisema kwa vile eneo hili limezungukwa na baadhi ya nchi zilizokumbwa na ugonjwa huo kunahitajika watu kufahamu namna ya kujikinga na ugonjwa huo.

Amesema wahudumu wa Afya ndiyo kundi sahihi ambalo linakaa na jamii hivyo kupata uelewa mpana kuhusiana na ugonjwa huo kuwawezesha wananchi kuepukana na ugonjwa huo hatari.

Urassa amesema hadi sasa nchi yetu haijapata ugonjwa huo hata hivyo kujikinga ni njia bora zaidi ya jamii kufahamu ili kuzuia maambukizi yake yasiweze kutokea.

“Namba ya simu ya dharura ni 199 hivyo mnapoona kuna mtu ana dalili pigeni ili msaada wa Afya utolewe kwa haraka,”amesema Urassa.

Amewataka wananchi kujiepusha na ulaji wa nyama za wanyama pori kwani ugonjwa huo unatokana na kundi hilo hususani nyani, tumbili, sokwe na panya.

Naye Kaimu Mganga Mkuu Mkoani Mwanza Stella Mwakibunga amesema wahudumu wa Afya ngazi ya jamii I watu wa kwanza katika utoaji wa msaada wa Afya hivyo uelewa juu ya elimu ya kujikinga na ugonjwa huo ni mhimu kwao.

Amewataka wawe wepesi kutoa taarifa ya tetesi za kuhusiana na ugonjwa huo pamoja na maradhi mengone ili jamii waliyonayo iweze kuwa na Afya bora ili waendelee na shughuli za uzalishaji mali.

Kwa upande wake Mhudumu wa Afya ngazi ya jamii kutoka kata ya Buhongwa wilayani Nyamagana Mwajuma Kavura alisema anashukuru kuwezeshwa juu ya elimu ya ugonjwa wa Mpox ili waelimishe jamii kujihadhari nao.

Amesema ugonjwa huo ambao umeanza kusambaa sehemu mbalimbali Duniani unapashwa kuepukwa kwani madhara yake yanaweza kuathiri jamii yetu kwani tuko karibu nchi ambazo ndo chimbuko la ugonjwa huo.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here