Home KITAIFA MAREKANI YAZIPA KAMPUNI TISA NCHINI DOLA MILIONI 8.3 .

MAREKANI YAZIPA KAMPUNI TISA NCHINI DOLA MILIONI 8.3 .

Dar es Salaam

SERIKALI ya Marekani kupitia Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la (USAID), limetangaza kuwekeza dola za Kimarekani milioni 8.3 kwa kampuni tisa za Tanzania ili kukuza biashara, kuboresha usalama wa chakula na kuimarisha ushindani.

Pia msaada huo utaiwezesha Tanzania kuongeza ushindani katika mauzo ya nje kupitia Mpango wa Ukuaji na Fursa Afrika (AGOA).

Hayo aliyasema leo Agosti 20 2024 jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi wa Mipango USAID/Tanzania, Craig Hart, wakati wa hafla ya maonyesho ya shughuli za biashara na uwekezaji ya USAID Afrika ambayo ilihudhuriwa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk. Selemani Jafo.

“Leo tunasherehekea ushirikiano wa USAID na kampuni tisa katika sekta muhimu zikiwemo asali, korosho na nguo. Ushirikiano huu unatarajiwa kuzalisha ajira 2,000, kuongeza dola milioni 42.5 katika mauzo mapya nje ya nchi na kukuza nafasi ya Tanzania kama kitovu cha uchumi wa kanda,” alisema.

Ametaja kampuni tisa za ndani zitapata ruzuku chini ya Mradi wa Biashara na Uwekezaji wa USAID Afrika na alitaja kampuni hizo kuwa ni BioBuu, Biotan Limited, Central Park Bees, Minjingu Mines and Fertilizer Limited, Mount Meru Millers, Red Earth Limited, Sabayi Investments Limited, Tanzania Tooku, Garments Co. Ltd na Mtu wa Tatu (Love Honey).

“Tunafungua njia kwa Tanzania kuwa kikapu cha chakula kikanda, muuzaji nishati nje, na kitovu cha ubunifu unaoendeshwa na vijana, na kupitia AGOA tunasaidia kampuni za Kitanzania kupata masoko Marekani,” amesema.

Hart amesema AGOA ni sehemu muhimu ya sera ya kiuchumi ya Marekani na Afrika inayozipa nchi zilizo chini ya Jangwa la Sahara kuuza bila ushuru kwa soko la Marekani kwa zaidi ya bidhaa 1,800.

Amesema Tanzania imejipanga vyema kupanua uzalishaji wake wa asali kwani kwa sasa ni nchi ya pili barani Afrika kwa uzalishaji wa asali na muuzaji mkuu wa Ulaya na kuongeza kuwa kampuni ya Man Limited (Upendo Honey) kwa kushirikiana na USAID inalenga kuongeza mauzo ya asali nje ya nchi kwa asilimia 767.

Kwa upande wake Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk.Seleman Jafo, amesema mradi wa Biashara na Uwekezaji wa USAID Afrika (ATI) umekuwa chachu katika kukuza uchumi na kuboresha maisha ya watu wa Tanzania.

“Onyesho hili la shughuli za mradi wa ATI ni ushuhuda wa dhamira yetu ya pamoja za kufungua fursa kubwa za uchumi wa Tanzania kupitia ongezeko la biashara na uwekezaji kwa kuwawezesha wafanyabiashara na kukuza ubunifu katika sekta muhimu za uchumi wetu,” amesema Dk.Jafo.

Amesema kupitia shughuli hizo Tanzania imeshuhudia ongezeko la mauzo ya baadhi ya bidhaa zinazouzwa nje ya nchi chini ya usaidizi, uzalishaji wa ajira mpya, na uwezeshaji wa wajasiriamali ambao sasa wanachangia kuimarika kwa uchumi wa nchi.

“Tunapoangalia sekta zinazosaidiwa kupitia Mradi wa ATI, tuna matumaini makubwa kwamba, hata mauzo yetu ya nje chini ya mpango wa AGOA yataongezeka sana wakati mipango yote itakapotekelezwa vyema.

“Nafahamu mijadala inayoendelea kati ya Wizara yangu na USAID kupitia mradi wa ATI wa AGOA na Youth Support, na ikifanikiwa kama ninavyotarajia, wakati ujao tutawaleta walengwa wetu ili kuonyesha mafanikio yao,” amesema.

Amesema wakati Tanzania ikisherehekea mafanikio kupitia Mradi wa ATI bado kuna kazi kubwa ya kutumia kikamilifu fursa za biashara na uwekezaji.

Amesema kuna haja ya kuendelea kukuza na kuimarisha uwezo wa uzalishaji na usambazaji ili kukidhi mahitaji ya soko, kupanua kapu la mauzo ya nje kwa kupanua zaidi ya sekta za jadi ili kujumuisha bidhaa zilizoongezwa thamani na zenye viwango vya juu.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here