Home KITAIFA DK.BITEKO AIPONGEZA EWURA KWA MWONGOZO WA USIMAMIZI WA USAFI WA MAZINGIRA NA...

DK.BITEKO AIPONGEZA EWURA KWA MWONGOZO WA USIMAMIZI WA USAFI WA MAZINGIRA NA TOPEKINYESI

• Asisitiza Ushirikiano wa Wadau katika usafi wa Mazingira nchini
•   Azitaka Mamlaka  kuweka mikakati  madhubuti ya usimamizi wa usafi wa mazingira

Dodoma

NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto Mashaka Biteko Agosti, 20 2024, ameipongeza Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kwa kuandaa Mwongozo wa Usimamizi wa Usafi wa Mazingira na Topekinyesi unaolenga kujenga jamii yenye afya bora na mazingira salama kwa kizazi cha sasa na kijacho.

Katika hotuba ya Ufunguzi wa Kongamano la Kitaifa la Usafi wa Mazingira, iliyosomwa kwa niaba yake na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), MWilliam Lukuvi, Dk.Biteko.

“Naipongeza EWURA kwa kuja na mwongozo huu wa Kiswahili ambao unalenga kuziongoza mamlaka za majisafi na usafi wa mazingira kutoa huduma ya usimamizi wa tope kinyesi kwa wananchi walio nje ya mtandao wa majitaka,”amesema

Aidha, Biteko, ameipongeza EWURA kwa kuboresha mfumo wa uwasilishaji taarifa za mamlaka hizo ( MajiS),ambao utatoa fursa ya kupata takwimu sahihi zaidi kuhusu usafi wa mazingira zitakazosaidia mipango ya maendeleo hususan katika sekta ya maji, afya na mazingira.

Mwongozo huu unawalenga wadau kama mamlaka za serikali za mitaa, sekta binafsi zinazotoa huduma ya usafi wa mazingira kwenye maeneo yasiyo na mtandao wa majitaka, wizara zenye dhamana, RUWASA na NEMC.

Taarifa ya EWURA ya utendaji wa mamlaka hizo kwa mwaka 2022/23, inaonesha ni mamlaka 21 tu kati ya 85 sawa na asilimia 24.7 ndizo zenye miundombinu ya kutibu majitaka na tope kinyesi kwa kipindi hicho.

Aidha, taarifa za Wizara ya Maji zinaonesha hadi Aprili, 2024 mtandao wa majitaka nchini ulikuwa kilometa 1455.93 ikilingalishwa na kilometa 1416.9 za Aprili, 2023. Idadi ya maunganisho katika mtandao, usafirishaji na kutibu majitaka umefikia kilometa 58,650 kutoka 56, 923 kwa kipindi kama hicho kwa mwaka uliopita.

“Yatupasa kufahamu kuwa ajenda ya usafi wa mazingira ni mtambuka na ndio maana hata sera zetu za afya, maji na mazingira zote zinasisitiza suala hili la usafi wa mazingira, nina Imani kongamano hili litaitendea haki ajenda ya usafi wa mazingira kwa kuja na mawazo chanya yenye lengo la kuboresha usafi wa mazingira nchini ili kuchochea maendeleo ya watu,” amesema.

Naye, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso ameipongeza EWURA kwa kuwakutanisha wadau mbalimbali kujadili namna ya kuimarisha masuala ya usimamizi wa mazingira kwa kwamba kuzinduliwa kwa mwongozo itazisaidia mamlaka za maji na wadau mbalimbali katika usimamizi wa huduma za usafi wa mazingira na tope kinyesi kuongeza ufanisi zaidi

Aweso amezikumbusha Mamlaka za Maji nchini kuzingatia mwongozo huo ambao umeweka misingi,mipaka, wajibu na majukumu ya utoaji huduma za usimamizi wa tope kinyesi zinazofanywa na mamlaka hizo.

“Ni vyema mnyororo wa huduma za usafi wa mazingira kuanzia kukusanya, usafirishaji na matumizi ya tope kinyesi ukazingatiwa ili kulinda afya za wananchi,” amesema.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Dk. James Andilile, amesema tathmini na tafiti zilizofanywa toka karne ya 19, zilibainisha kuwa watu wanapokaa kwenye mazingira safi, afya zinakuwa imara na ni njia ya kujikinga na magonjwa mengi.

“Tumeona tukusanyike na tutafakari na kupanga mikakati ya pamoja ya kuboresha usafi wa mazingira,”amesema.

Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya EWURA, Victoria Elangwa alisema katika kongamano hilo kutakuwa na mawasilisho mbambali yatakayosaida wataalam kuchakata namna bora ya kutunza mazingira na kuahidi kwamba Bodi hiyo itayasimamia.

Mwisho.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here