Home KITAIFA WADAU WA UJENZI WASHAURIWA KUTUMIA MAABARA ZA TARURA

WADAU WA UJENZI WASHAURIWA KUTUMIA MAABARA ZA TARURA

Dodoma

WADAU wa ujenzi wa miundombinu ikiwemo barabara, madaraja, makalavati na majengo nchini wameshauriwa kutumia Maabara za Wakala Rural wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) ambazo zipo katika MIKOA 11 nchini ili kujenga miundombinu yenye ubora.

Rai hiyo imetolewa leo Agosti, 6 2024 na Fundi Sanifu Mkuu wa Maabara ya TARURA, Jacob Manguye wakati akitoa elimu kwa wananchi waliofika katika Banda la TARURA kwenye maonesho ya Kitaifa ya Nane Nane yanayoendelea kwenye Viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma.

Amesema kutopeleka sampuli za vifaa vya ujenzi kwenye Maabara husababisha hasara kwa mwenye kazi na kwa serikali.

TARURA ilianzisha Maabara kwaajili ya kupima vifaa vya ujenzi za kampuni na watu binafsi na kwa kazi za barabara zinazo simamiwa na TARURA zinazotekelezwa vijijini na mijini ikiwa na lengo la kusimamia ubora na ufanisi wa miundombinu ya barabara na sekta nyingine za ujenzi.

Ameongeza kuwa hadi sasa wanazo Maabara kumi na moja (11) zilizosajiliwa na zinafanya kazi kwa ufanisi mkubwa katika mikoa ya Dodoma, Mbeya, Geita, Kigoma, Simiyu, Tanga, Mtwara, Mwanza, Ruvuma, Morogoro pamoja na Arusha.

Amesema lengo la TARURA ni kuwa na Maabara katika MIKOA yote nchini ili kuweza kupima ubora wa sampuli zinazotumika kujenga miundombinu kama vile udongo,lami au kokoto kutoka kwa wadau wanaotekeleza miradi yao ya ujenzi nchini.

Kwa upande mwingine Mangunye amewaomba watumiaji wa barabara nchini hususan madereva wa vyombo vya moto kufuata sheria za barabarani kwa kutopitisha magari yenye uzito mkubwa kupita ule unaoruhusiwa ili kuzilinda barabara zidumu muda mrefu.

Aidha, amewaomba wananchi kuacha kufanya shughuli za kibinadamu pembezoni ya barabara ikiwemo shughuli za kilimo na ufugaji ili kuepusha uharibifu unaweza kutokea kwenye barabara husika.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here