Home KITAIFA SERIKALI IMESEMA SEKTA YA KILIMO NI CHANZO NA MHIMILI MKUBWA KATIKA AJIRA

SERIKALI IMESEMA SEKTA YA KILIMO NI CHANZO NA MHIMILI MKUBWA KATIKA AJIRA

Esther Mnyika, Dodoma

SERIKALI imesema sekta ya kilimo ni chanzo na muhimili mkubwa katika ajira, kwa vijana,ambapo kwa mujibu wa taarifa ya utafiti wa nguvu kazi nchini ya mwaka 2020/2021 ni asilimia 54.8 ya idadi ya watu wote nchini. Hiyo ni sawa na watu milioni 34.

Waziri wa Nchi,Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji,Profesa Kitila Mkumbo.

Hayo yamebainishwa leo Agosti, 6 2024 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo wakati akifungua Kongamano la uwekezaji katika sekta za utalii, kilimo lilofanyika kwenye maonesho ya Kimataifa ya Kilimo Nanenane yanayoendelea Viwanja vya Nzuguni Jijini Dodoma.

Amesema kila mwaka, tarehe nane mwezi wa nane, nchi huadhimisha siku ya wakulima kwa kutambua mchango wao mkubwa katika uhai wa Taifa letu na maendeleo ya nchi kwa ujumla.

“Sekta ya kilimo katika maisha na maendeleo ya nchi yetu ni dhahiri. Kwanza, kilimo ndicho kinachotupa chakula, ambayo ni hatua ya kwanza katika maisha ya binadamu. Pili, sekta ya kilimo inachangia asilimia 26 ya pato la taifa. Hii inamaanisha kuwa katika pato la taifa la shilingi trilioni 148.7 trilioni 38 zinatokana na sekta za kilimo. wanajishughulisha kikamilifu na shughuli za kiuchumi (economically active population), ambapo asilimia 65 wanajishughulisha na shughuli katika sekta ya kilimo, uvuvi na ufugaji,”amesema.

Ameeleza kuwa mpango wao wa maendeleo wa mwaka 2024/2025 wana maeneo kumi yaliyopewa msukumo na baadhi ya maeneo hayo ni pamoja kuendelea kuwekeza katika kukuza uzalishaji katika sekta ya kilimo.

“Kuendelea kuhamasisha na kuwezesha matumizi ya mbegu bora, matumizi ya mbolea, kilimo cha umwagiliaji na matumizi ya zana za kisasa katika kilimo. Kama tunavyofahamu, uchumi wa viwanda tunaojaribu kuujenga malighafi zake nyingi (65%) zinategemea kilimo,” amesema

Profesa Mkumbo katika kipindi cha muda mfupi na muda wa kati, watanzania wengi wataendelea kuajiriwa na kujiajiri katika sekta ya kilimo.

Amefafanua sehemu ya pili ni kuchochea na kuvutia uwekezaji katika viwanda vyenye kulenga kuzalisha bidhaa zitakazoifanya nchi jitosheleze kwa mahitaji ya bidhaa muhimu nchini na kukuza mauzo ya bidhaa zilizoongezwa thamani nje ya nchi.

“Tunaagiza bidhaa kutoka nje ya nchi. Bidhaa hizi ni pamoja na mafuta ya kula, sukari, ngano, n.k. Aidha, mauzo yetu nje ya nchi bado yametawaliwa kwa kiasi kikubwa na bidhaa ambazo hazijaongezwa thamani. Eneo la tatu ni kuendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji ili kuchochea ukuaji wa sekta binafsi, hususan tukilenga kuweka mazingira maalum ya kukuza na kuimarisha biashara na uwekezaji katika sekta ya biashara ndogo na ya kati (small and medium enterprises),”amesema.

Akizungumzia kuhusu Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) Profesa Mkumbo amesema mujibu wa takwimu zaTIC sekta tano zinavutia zaidi uwekezaji nchini ni uzalishaji viwandani, usafiri na usafirishaji, ujenzi wa majengo ya biashara, utalii na kilimo.

“Kwa kuzingatia idadi ya miradi inayosajiliwa na TIC (2021-2024), kati ya miradi 1484 iliyosajiliwa katika kipindi hiki, uzalishaji viwandani unaongoza (608, 41%), ukifuatiwa na usafiri na usafirishaji (262, 17.6%), utalii (142, 9.5%) majengo ya biashara (140, 9.4%), na kilimo (123, 8.3%). Hata hivyo, kwa kuzingatia idadi ya ajira zinazozalishwa na miradi ya uwekezaji kilimo kinaongoza.

“Kati ya ajira 353,133 zilizotarajiwa kuzalishwa kutokana na miradi ya uwekezaji katika kipindi tajwa jumla ya ajira 115,212 (32.7%) zilitokana na kilimo, ikifuatiwa na viwanda (95,397, 27%), usafiri na usafirishaji (39,230, 11.1%), majengo ya biashara (11,212, 3.2%) na utalii (10,266 (2.9%),” amesema.

Kwa upande wake Waziri Mkuu Mstaafu, Mizengo Pinda amesema kwenye kongamano hilo wawasikilize wataalamu nini kifanyike katika kuendeleza kilimo na uzalishaji bora wa mazao.

“Niwapongeze mlioandaa kongamano hili kwaajili ya kutoa utalaamu kutoka kwa wataalamu mbalimbali japo bado kuna tatizo hattujui jinsi gani ya kutumia fursa,” amesema Pinda.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here