Home BURUDANI TAMASHA LA UTALII LUSHOTO KUIBUA FURSA MPYA ZA AJIRA KWA WANANCHI

TAMASHA LA UTALII LUSHOTO KUIBUA FURSA MPYA ZA AJIRA KWA WANANCHI

Na Ashrack Miraji, Tanga

MKUU wa Wilaya Lushoto, Japhari Kubecha, amesema Tamasha la Utalii Wilayani humo liitwalo USAMBALA TOURISM FESTIVAL linatarajiwa kufanyika mwezi Septemba mwaka huu ambapo litaibua fursa za ajira kwa wananchi wa Wilaya hiyo pamoja na kutangaza vivutio vingi vya utalii vilivyopo katika eneo hilo.

Akizungumzia tamasha hilo linalotarajia kufanyika Kwa siku mbili za Septemba 6 hadi 7 Mkuu huyo wa Wilaya ya Lushoto amesema pamoja na kuwa ni tamasha la utalii lakini pia litaibua fursa mbalimbali za ajira pamoja na uwekezaji ndani ya wiilaya hiyo.

Kubecha amewataka wananchi wilayani hapo kutumia nafasi hiyo katika kutangaza bidhaa zao hususani bidhaa za asili ili kuwavutia watalii watakaofika kwenye tamasha hilo.

“Tumeandaa tamasha hili kubwa la utalii wilayani Lushoto,lengo letu ni kuunga mkono jitihada za Rais Dk.Samia Suluhu Hassan ambaye hivi karibuni amezindua filamu ya Royal Tour kwa lengo la kutangaza vivutio vya utalii nchini na tumeona matokeo yake chanya hivyo basi kama wilaya tumeamua kumuunga mkono Rais wetu kwa kufanya tamasha hili ambalo litaibua hisia za watanzania walio wengi na kumtambua Mhe Rais kama kinara wa utalii Tanzania,” amesema kubecha.

Amesema tamasha hilo pia linalenga kufungua fursa kwa wawekezaji mbalimbali hapa nchini kuja kuwekeza katika wilaya ya Lushoto ambayo ina rasilimali mbalimbali ikiwemo kilimo Cha mboga mboga,upandaji miti ya mbao,uchimbaji madini ili kujenga vivutio mbalimbalimbali vya utalii ambavyo vyote hivi vitakuwa ni fursa kwa vijana kujipatia ajira na kuongeza pato la Taifa.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here