Home KITAIFA DK.SAMIA AAGIZA MRADI WA CHUMA LIGANGA KUANZA UZALISHAJI

DK.SAMIA AAGIZA MRADI WA CHUMA LIGANGA KUANZA UZALISHAJI

Na Esther Mnyika @@Lajiji Digital

RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan amewaagiza Waziri wa Viwanda na Biashara Dk. Ashatu Kijaji na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais,  Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo  kuhakikisha mradi  wa chuma wa Liganga  unaanza uzalishaji  na malighafi hiyo itumike kwenye viwanda vya hapa nchini. 

Akizungumza leo Mei, 9, 2024  jijini Dar es Salaam, Dk. Samia wakati akizindua kiwanda cha kuunganisha malori na matipa cha Surtun  kilichopo Kisarawe II  Wilaya ya Kigamboni ambao  umehudhuriwa  na viongozi mbalimbali wa Serikali,Taasisi,  Dini na wengine.

Amesema malighafi zinazopatikana  katika mradi wa chuma wa Liganga  utasaidia  utengenezaji wa vipuri na bidhaa nyingine zinazozalishwa na viwanda vya ndani. 

“Mradi huu ni muhimu kwa uchumi  wa viwanda  vya chuma na mhakikishe mnapata mwekezaji mzuri atakayechimba chuma hiki na kisha kitumike kwenye viwanda vingine,”amesema Dk.Samia.

Amesema  serikali itaendelea  kujenga  uchumi  wa kisasa  funganishi na jumuishi  na shindani katika  msingi  wa viwanda,  huduma  za kiuchumi  na miundombinu wezeshi.

Amesema  sekta  ya viwanda inaongoza uzalishaji  na kutoa ajira kwa wananchi jambo ambalo ni muhimu  katika  kukuza kusaidia katika mapambano ya kuondoa umaskini.

Dk. Samia  amesema   serikali  imepunguza kodi ya makapuni kutoka asilimia 30 hadi asilimia 10 kwa kipindi  cha miaka  mitano ya mwanzo ili kuchochea  uwekezaji  zaidi kwenye  sekta ya viwanda.

“Kiwanda hiki ni chachu ya ukuaji wa viwanda na sekta nyingine  kwa kuwa  kutumia vioo vinavyozalishwa na kiwanda kingine ambacho zaidi ya asilimia 89 ya malighafi  zake zinapatikana hapa nchini,”amesema. 

Pia Dk. Samia  amesema  matumizi  ya bidhaa zinazozalishwa nchini zinapunguza gharama  kwa kampuni zenyewe zinazotengeneza magari na inaongeza manufaa ya uwepo wa kampuni  hiyo kwa uchumi  wa nchi.

Ameongeza  kuwa kiwanda hicho kimetoa ajira  za moja kwa moja 250 na zisizo rasmi  1800 kuongeza  mzunguko wa fedha, mapato ya serikali  na kuimarisha teknolojia.

Naye Waziri wa Viwanda na Biashara Dk.Ashatu Kijaji,  amesema  serikali imechukua uamuzi   wa kulipa fidia wananchi wanaozunguka mradi wa madini  ya vioo wa Engaruka uliopo Wilaya ya Monduli mkoani Arusha.

Amesema  malighafi zitakazopatikana katika  mradi huo zitatosheleza kwa zaidi ya asilimia 99 ya viwanda  vya vioo hapa nchini.

“Mradi huu ni muhimu kwa uchumi  wa viwanda vya vioo na kwamba hakutakuwa na haja ya kuagiza malighafi  nje ya nchi,”amesema Dk.  Kijaji.

Amesema  hatua hiyo ya serikali  ni ushindi mkubwa kwa uwekezaji na uzalishaji wa bidhaa za vioo hasa viwanda vilivyopo nchini.

Aidha amesema sekta  ya viwanda  imeajiri watu kutokana na kufanya  marekebisho ya sheria,  kanuni,  miongozo kwa ajili  ya wawekezaji. 

Naye Waziri  wa Nchi Ofisi ya Rais Mpango  na Uwekezaji , Profesa Kitila Mkumbo amesema katika miaka mitatu iliyopita uchumi wa Tanzania  umekua na kuimarika  ukikua kwa asilimia sita

Amesema  uchumi  wa Tanzania  umeimarika  kutokana na uwekezaji  uliofanywa  na serikali katika  kilimo na ujenzi  wa miundombinu.

“Sekta ya  viwanda  imekuwa na mchango   wa asilimia 10 katika  miongo mitatu iliyopita lakini  kwa sasa changamoto nyingi  zimetatuliwa na ndio maana  uwekezaji  katika sekta hii unazidi kukua,”amesema Profesa Kitila.

Amesema  kati miradi 526 iliyosajiliwa na Kituo cha Uwekezaji Tanzania kwa mwaka jana, pekee na miradi 237 iliikuwa ni ya uzalishaji  viwandani.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni  ya Surtun  Corporation Limited,Rehmtullah Habib amesema  ni  cha kuunganisha  magari aina kuu mbili malori na matipa  na kwa siku kuzalisha malori 30 na matipa tisa.

Amesema hadi sasa wamezalisha magari  150 na wanazalisha aina kuu mbili ambazo malori na matipa kwa ajili ya shughuli mbalimbali katika sekta ya ujenzi na madini.

” Kiwanda hiki kimeajiri watu 250 na ajirazisizo rasmi 1800 wakati tunaanza kuuza magari walikuwa 20 tangu kiwanda kianze ajira  zimeongeza,”amesema Habib.

Aidha amesema bado wanahitaji kujenga kiwanda cha vipuri  hivyo wameomba eneo la hekari 54 kwa ajili  ya kiwanda  hicho.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here