Home KIMATAIFA TANZANIA YAISHAURI BENKI YA DUNIA KUWEKA VIPAUMBELE KATIKA MIRADI YA MAENDELEO AFRIKA

TANZANIA YAISHAURI BENKI YA DUNIA KUWEKA VIPAUMBELE KATIKA MIRADI YA MAENDELEO AFRIKA

Na Scola Malinga, WF, Washington

TANZANIA imeishauri Benki ya Dunia kutilia maanani vipaumbele vya maendeleo vya nchi za Afrika ikiwemo kuzipatia fedha na ujuzi ili ziweze kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo. 

Rai hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dk. Natu El-maamry Mwamba kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Dk. Mwigulu  Nchemba , kwenye Mkutano wa Mawaziri wa Fedha na Magavana wa Kundi la Kwanza la Nchi za Afrika la Benki ya Dunia) (WBG Africa Group 1 Constituency) uliofanyika Washington DC, nchini Marekani.

Amesema kuwa Benki ya Dunia imekuwa inasaidia kwa kiasi kikubwa nchi za Afrika na sasa wasaidie kuwekeza nguvu zaidi kwenye miradi ya Maendeleo ili kuinua uchumi kwa haraka.

“Tunaiomba Benki ya Dunia inapopitia   matarajio yao iweke  kipaumbele kwa Afrika na kwa nchi moja moja na kutoa nyongeza ya rasilimali fedha,” amsema Dk. Mwamba.

Aidha, Dk. Mwamba ameiomba Benki ya Dunia kupeleka fedha zitakazoongezwa kupitia mzunguko mpya wa Mfuko wa IDA 21 zipelekwe moja kwa moja kwa walengwa ili kupata matokeo chanya kwa haraka.Aidha, ametoa wito kwa Mashirika ya Fedha ya Kimataifa kutoa mikopo ya muda mrefu (Long Term Loans) isiyo na riba ili nchi za Afrika ziweze kutekeleza miradi ya maendeleo kikamilifu.

“Mikopo ya muda mfupi inaumiza nchi za Afrika, hivyo tunaomba mikopo iwe ya muda mrefu, miaka 50 hadi 70 na isiyo na riba,” amesisitiza Dk. Mwamba. 
 

Dk. Mwamba ametumia nafasi hiyo kuwakumbusha ombi la Serikali ya Tanzania katika Mkutano wa 26 wa Kundi la Kwanza la Nchi za  Afrika uliofanyika Marrakech, Morocco mwaka jana, la kukifanya kiswahili kuwa miongoni wa lugha za mawasiliano wakati wa mikutano yake kutokana na kukua kwa lugha hiyo na kutumika kwenye mikutano mingine mingi ya Kikanda na Kimataifa.

“Kiswahili kimekuwa moja ya lugha inayotumika katika mikutano ya  Afrika Mashariki (EAC), SADC, AU na sasa inakwenda kupitishwa kutumika kwenye mikutano ya kimataifa,” amesema.

Mkutano huo ulihudhuriwa na nchi 22 wanachama ikiwa ni pamoja na Tanzania, Botswana, Burundi, Eritrea, Eswatini, Ethiopia, Gambia, Kenya, Lesotho, Liberia, Malawi, Msumbiji, Namibia, Rwanda, Ushelisheli, Sierra Leone, Somalia, Sudan, Sudan ya Kusini,Uganda, Zambia, na Zimbabwe.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here