Home KITAIFA TANZANIA NA IVORY COAST ZAINGIA RASMI MAKUBALIANO YA USHIRIKIANO KWENYE SEKTA YA...

TANZANIA NA IVORY COAST ZAINGIA RASMI MAKUBALIANO YA USHIRIKIANO KWENYE SEKTA YA MICHEZO

Na, Brown Jonas WUSM, Dar es Salaam.

WIZARA ya Utamaduni, Sanaa na Michezo imeingia makubaliano ya ushirikiano na Wizara ya Michezo ya Ivory coast katika masuala mbalimbali ya uendelezaji wa Sekta ya michezo.

Makubaliano hayo yameingiwa leo Aprili 21, 2024 Jijini Dar Es Salaam ambapo Naibu Waziri Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa upande wa Tanzania, Hamis Mwinjuma amesaini makubaliano hayo kwa niaba ya Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Dk. Damas Ndumbaro huku Ivory Coast aliyesaini makubaliano hayo ni Waziri wa Michezo wa nchi hiyo Adjé Silas.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo Mwinjuma amesema makubaliano hayo yatajikita kwenye uandaaji wa miundombinu ya michezo, uandaaji wa timu kuelekea michuano ya AFCON 2027 itakayofanyika nchini Tanzania kwa kushirikiana na Kenya na Uganda.

“Sisi na Ivory Coast tutashirikiana kwenye maeneo tofauti kwa kuwa tunafanana kwenye mazingira mengi, hivyo ni bora kujifunza kwa mtu unaefanana nae kuliko kwenda kuchukua watu wa dunia ya kwanza waje kukufundisha vitu ambavyo itakua ngumu kuvifanya,” amesisitiza Mwinjuma.

Hafla hiyo imehudhuriwa na Katibu Mkuu, Gerson Msigwa, Naibu katibu Mkuu Dk. Suleiman Serera Kaimu Mkurugenzi Idara ya maendeleo ya Michezo Ally Mayay, Katibu Mtendaji wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Neema Msitha, Katibu Mtendaji wa Baraza la Sanaa la Taifa Dk. Kedmon Mapana pamoja na Maofisa wa nchi hizo mbili.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here