Home KITAIFA Kamishina Kiiza – Kuweni mabalozi wa kuisemea Serikali katika zoezi la kuhama...

Kamishina Kiiza – Kuweni mabalozi wa kuisemea Serikali katika zoezi la kuhama Ngorongoro

Na John Mapepele

Wananchi wanaopisha uhifadhi kwa hiari katika Hifadhi ya Ngorongoro kwenda kuishi maeneo mengine wametakiwa kuwa mabalozi wa kuwekeza mema yanayofanywa na Serikali katika kuboresha maisha yao kwa wananchi waliobaki.

Kauli hiyo imetolewa Machi 3, 2024 na Kamishina Richard Kiiza katika ofisi ya zamani ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kwenye hafla ya kuaga wakazi zaidi ya 450 na mifugo 1259 wanaoondoka kwenda Msomera Tanga na Meatu mkoani Simiyu.

” Ninawasihi muendelee kuwa mabalozi wa kulisemea zoezi hili la kuhamisha wenyeji kwa hiari na kuwaelimisha wengine ambao bado hawajajiandikisha kwa kuwapa taarifa sahihi ili na wao waweze kufanya maamuzi sahihi kama mlivyofanya ninyi,” amesisitiza Kamishina Kiiza.

Amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan umedhamiria kuboresha maisha ya wananchi wake ili waondokane na changamoto za ndani ya wanyama ndani ya Hifadhi.

Amewapongeza wenyeji hao kwa kuhamasika na kuamua kuhama kwa hiari ambapo amefafanua kuwa uamuzi huo unatoa fursa ya kuendeleza uhifadhi kwa manufaa ya Taifa na pia kuwapa fursa ya kuwa na maisha bora zaidi nje ya Hifadhi.

Aidha, ametoa wito kwa wanaohamia eneo la Msomera kutumia vizuri ardhi waliyopewa na Serikali pamoja na fedha kufanya shughuli za maendeleo.

Msemaji wa Wizara ya Maliasili na Utalii, John Mapepele amefafanua kuwa Serikali itaendelea kuhakikisha kila kaya inayokubali kuhama kwa hiari kupewa haki na stahili zote kwa mujibu wa taratibu za zoezi hili ikiwa ni pamoja na kulipwa fidia ya maendelezo, kulipwa milioni kumi za Rais Samia Suluhu Hassan, kupewa nyumba, kiwanja cha ziada na kusafirishwa mizigo yao hadi Msomera au maeneo mengine waliyoyachagua.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here